POLISI KANDA MAALUMU YA DSM YAWATEMBELEA ASKARI WALIOKO KIBITI, RUFIJI NA KUWAFARIJI KWA ZAWADI KIBAO ZA SIKUKUU - MUKAMAFUNNY BLOG

Breaking

Home Top Ad

Post Top Ad

Wednesday, January 3, 2018

POLISI KANDA MAALUMU YA DSM YAWATEMBELEA ASKARI WALIOKO KIBITI, RUFIJI NA KUWAFARIJI KWA ZAWADI KIBAO ZA SIKUKUU



Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam imetembelea Mkoa wa Rufiji katika utaratibu wa kawaida wa jeshi hilo wa kuimarisha ujirani mwema na kubadilishana uzoefu.

Makamanda wa polisi wa mikoa inayounda Kanda Maalumu ya Dar es Salaam wakiongozwa na Kamanda wa kanda hiyo, Lazaro Mambosasa walifika Mkoa wa Kipolisi wa Rufiji jana Jumanne Januari 2,2018 na kupokelewa na kamanda wa mkoa huo, Onesmo Lyanga.

Msafara wa Kamanda Mambosasa ulibeba zawadi za sikukuu kwa ajili ya askari ambao wapo katika operesheni maalumu katika eneo hilo ambalo siku za nyuma liligubikwa na matukio ya mauaji ya wananchi wasio na hatia na askari.

Akizungumza na baadhi ya askari waliopo Rufiji, Kamanda Mambosasa amewapongeza kwa kufanya kazi kwa uzalendo na kwa kufuata kiapo chao licha ya mazingira ya kazi si rafiki.

"Hakuna asiyejua hali iliyokuwepo Rufiji mpaka wananchi wakakata tamaa na wengine walihama lakini kamanda mwenzangu ameniambia hali sasa ni shwari, Dar es Salaam tuko pamoja na ninyi na tunathamini kazi mnayoifanya. Usalama wa Dar es Salaam unategemea kwa kiasi kikubwa usalama wa hapa pia," amesema Kamanda Mambosasa.

Amesema hali ya usalama Dar es Salaam ni shwari na askari hawajalala wapo imara kama walio kwenye operesheni hiyo kwa kuwa wahalifu wanaobanwa Pwani na kukimbilia Dar es Salaam hawabaki salama.

"Hatukuja Boxing day (siku ya kufungua zawadi) lakini leo tumewaletea ndafu, kidogo, kilo 200 za mchele, sukari, maji na mafuta, ninyi endeleeni kupeperusha bendera ya Jeshi la Polisi na haya mambo yatakwenda lakini baadaye yataisha,” amesema.

Kwa upande wake, Kamanda Lyanga amesema wamekuwa wakitembelewa na viongozi na watu wengine wengi, hivyo morali ya askari waliopo katika operesheni iko juu na wanafanya kazi kwa weledi na mpaka sasa hakuna malalamiko yoyote ya wananchi jambo ambalo linaashiria kuwa sheria zinafuatwa.

"Baada ya kuwa tumewafikia wahalifu sasa wananchi wanawapenda askari wao, wanatoa taarifa hawaogopi tena kama zamani," amesema Kamanda Lyanga.

No comments:

Post a Comment

Post Bottom Ad

Responsive Ads Here

Pages